kuhusu kunyakuliwa kwa kanisa la Kristo.
|  | 
| Bishop sylvester Gamanywa | 
Mada hii 
inaanza kwa kuchambua maana ya misamiati wa kunyakuliwa, jinsi tukio 
litakavyokuwa, sababu za kunyakuliwa; na mchakato wa maandalizi ya 
unyakuo wenyewe. Karibuni.
MAANA YA KUNYAKULIWA
"Kunyakuliwa" ni tukio maalum la kinabii ambalo linatarajiwa kutokea 
wakati wowote kwa ajili ya kuhitimisha huduma za Kanisa la Kristo 
duniani. Tukio hili linawahusu makundi mawili ya walengwa. Kundi la 
kwanza ni “kufufuliwa kwa wafu waliolala mauti katika Kristo”! Na kundi 
la pili ni “wanafunzi halisi wa Yesu Kristo tutakaokutwa hai. Na hii ni 
kwa mujibu wa maandiko ya Paulo alipowaandikia Wathesalonike:
"Lakini, ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala mauti, msije 
mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini. Maana, ikiwa twaamini ya
 kwamba Yesu alikufa akafufuka, vivyo hivyo na hao waliolala katika 
Yesu, Mungu atawaleta pamoja naye. Kwa kuwa twawaambieni haya kwa neno 
la Bwana, kwamba sisi tulio hai, tutakaosalia hata wakati wa kuja kwake 
Bwana, hakika hatutawatangulia wao waliokwisha kulala mauti. Kwa sababu 
Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya 
malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo 
watafufuliwa kwanza. Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa 
pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa 
pamoja na Bwana milele. Basi, farijianeni kwa maneno hayo." (1 THE. 
4:13-18)
JINSI UNYAKUO UTAKAVYOFANYIKA
Tukio hili la 
kinabii litafanyika kwa kasi na kwa kushtukiza. Hakutakuwepo na taarifa 
ya kujiandaa kwa unyakuo. Maandiko yanasema kwamba itakuwa ni: "kwa 
dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa parapanda ya mwisho; maana 
parapanda italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu, nasi 
tutabadilika." (1 KOR. 15:52)
Kwa sababu ya kushtukiza kwa tukio 
hili la ghafla imeandikwa ya kuwa kuna baadhi waliotakiwa kunyakuliwa 
wataachwa kwa sababu ni kwa ajili ya watakaokutwa wako tayari tu ndio 
watakaonyakuliwa:
"Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, 
ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. Kwa kuwa kama vile siku 
zile zilizokuwa kabla ya Gharika watu walivyokuwa wakila, na kunywa, 
wakioa na kuolewa, hata siku ile aliyoingia Nuhu katika safina, 
wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote, ndivyo kutakavyokuwa 
kuja kwake Mwana wa Adamu. Wakati ule watu wawili watakuwako kondeni; 
mmoja atwaliwa, mmoja aachwa; wanawake wawili watakuwa wakisaga; mmoja 
atwaliwa, mmoja aachwa.Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi 
atakayokuja Bwana wenu." (MT. 24:37-42)
SABABU ZA KUNYAKULIWA
Baada ya kupitia tafsiri na jinsi unyakuo utakavyofanyika, napenda 
tupitie hoja muhimu za sababu za kunyakuliwa. Napenda kuzielezea sababu 
hizi kwa sababu kuna malumbano ya kitheolojia kuhusu unyakuo na mjadala 
ukilenga ni wakati gani unyakuo utafanyika.
Kuna kundi lenye 
kudai kunyakuliwa kutafanyika kabla kuanza kipindi cha miaka 7 ya dhidi 
kuu (Pre-tri-rapture) ; kundi la pili linaamini unyakuo utafanyika 
katikati ya kipindi cha miaka 7(Mid-tri-rapture); na kundi jingine 
linaamini kunyakuliwa kutafanyika mwishoni mwa dhiki kuu 
(Post-tri-rapture)
Uchunguzi wangu na imani yangu vinaangukia 
katika kundi la kwanza la(Pre-tri-rapture) na ndiyo maana nimeona nitoe 
sababu za kunyakuliwa kabla ya kuanza kipindi cha dhiki kuu.
1. Ahadi ya Yesu Kristo
Yesu mwenyewe ndiye aliyetangulia kuwajulisha wanafunzi wake kuhusu 
suala la kurudi tena kuwachukua ili wakae pamoja naye mbinguni: " 
Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; 
maana naenda kuwaandalia mahali. Basi mimi nikienda na kuwaandalia 
mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi 
mwepo." (YN. 14:2-3)
2. Kuepushwa na ghadhabu ya Mungu
Mtume Paulo alidokeza habari za ujio wa Mpinga Kristo na atakavyotawala 
chini ya uvuvio wa Shetani mwenyewe. Na Kisha akataja habari za wale 
watakaochwa baada ya unyakuo watakavyoingia kwenye kipindi cha 
udanganyifu mkubwa wa Shetani kwa sababu walikataa kuamini kweli ya 
Injili kabla ya unyakuo:
“Hapo ndipo atakapofunuliwa yule asi, 
ambaye Bwana Yesu atamwua kwa pumzi ya kinywa chake, na kumwangamiza kwa
 ufunuo wa kuwapo kwake; yule ambaye kuja kwake ni kwa mfano wa kutenda 
kwake Shetani, kwa uwezo wote, na ishara na ajabu za uongo; na katika 
madanganyo yote ya udhalimu kwa hao wanaopotea; kwa sababu hawakukubali 
kuipenda ile kweli, wapate kuokolewa. Kwa hiyo Mungu awaletea nguvu ya 
upotevu, wauamini uongo; ili wahukumiwe wote ambao hawakuiamini kweli, 
bali walikuwa wakijifurahisha katika udhalimu.” (2 THE. 2:8-12)
Kwa hiyo, kunyakuliwa kabla ya kipindi cha utawala wa MpingaKristo ni 
ili tuepushwe na hii ghadhabu ya Mungu inayotarajiwa kuupata ulimwengu 
katika kipindi hicho: “Kwa kuwa wao wenyewe wanatangaza habari zetu, 
jinsi kulivyokuwa kuingia kwetu kwenu; na jinsi mlivyomgeukia Mungu 
mkaziacha sanamu, ili kumtumikia Mungu aliye hai, wa kweli; na kumngojea
 Mwanawe kutoka mbinguni, ambaye alimfufua katika wafu, naye ni Yesu, 
mwenye kutuokoa na ghadhabu itakayokuja.” (1 THE. 1:9-10)
TISHIO LA KUACHWA KAMA HAKUNA MAANDALIZI
Kufuatia tukio la kunyakuliwa kufanyika ghafla, ndiyo maana maandiko 
yanahimiza walengwa wa unyakuo kuwa tayari wakati wote ili wasijekuachwa
 wakati wa unyakuo. Na hii ndiyo sababu ya kuamini kwamba unyakuo 
utafanyika kabla ya kipindi cha dhiki kuu ili walengwa wawe wametimiza 
vigezo vya unyakuo huo wasijepatwa na mabalaa ya dhiki kuu.
Ushahidi ni maandiko yanayo tahadharisha kuwa tayari, kutubu na kuishi 
maisha ya utakaso kamili wakati wote: "Na ndani yake hakitaingia kamwe 
cho chote kilicho kinyonge, wala yeye afanyaye machukizo na uongo, bali 
wale walioandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo." (UFU. 
21:27)
Yesu mwenyewe aliyaonya makanisa ya Karne ya kwanza 
yajitakase na kujiweka tayari kwa unyakuo vinginevyo yatakosa fursa 
hiyo. Kwa Kanisa la Efeso alilionya akisema: "Basi, kumbuka ni wapi 
ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza. Lakini, usipofanya 
hivyo, naja kwako, nami nitakiondoa kinara chako katika mahali pake, 
usipotubu." (UFU. 2:5)
Maana ya "Kuondolewa kinara" ni kufutiwa 
haki ya urithi wa ufalme wa mbinguni na kufutwa jina kwenye kitabu cha 
uzima. Mtume Paulo naye anasisitiza akisema kwa kuwa siku ya unyakuo 
yaja kama mwivi na itawakumba wote wasiojiandaa;akasema sisi tusikubali 
kubaki gizani mpaka tuvamiwe ghafla:
“Maana ninyi wenyewe mnajua 
yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku. Wakati 
wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, 
kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa. Bali 
ninyi, ndugu, hammo gizani, hata siku ile iwapate kama mwivi.” (1 THE. 
5:2-4)
Tutaendelea na sehemu ya pili ambapo tutapitia mchakato wa
 maandalizi kwa ajili ya kunyakuliwa, ni mambo gani yatakayojiri baada 
ya unyakuo mbinguni na nini kitaendelea duniani. Tafadhali kama ujumbe 
huu umekugusa nijulishe kwa ku-like ukurasa huu na kisha warushie na 
marafiki zako wengine.
Sign up here with your email
 
1 comments:
Write commentsasante sana
ReplyConversionConversion EmoticonEmoticon